Friday, February 23, 2007

Kama Nabwa umekwenda, Unabwa umetuwachia

Na Mohammed Ghassani

Mwanzoni mwa asubuhi
Dunia inaamka
Malaika wa mauti akashuka
Baba akamkabili kumwambia:
“Nimetumwa na Molao
Mbeleye uhudhurie!”
Kwa sauti ya kupuma
Baba akamuuliza:
“Ni vipi wanangu, nani atawalea
Ni nani wa kuwatunza
Nani atawaongoza
Kupambana mapambano?”

Yule malaika akaamba:
“Uliishi uhai wako
Kwa hima ya kupambana
Ukazaa watoto wako
Kwa hima ya kupambana
Na sasa hivi waenda, wauliza mapambano?
Masikini Ali Nabwa, mja wa kupambana
Hebu tuende kwa Mola
Siku sasa imefika
Urudi ukapumue!”

Baba naye akajibu:
“Kurudi kwa Bwana’ngu,
Sipingi, sipingi katu
Hiyino faradhi yangu
Walakini khofu yangu
Ni hawa vijana wangu
Wataweza mapambano
Wataishi kimapambano
Kisha wafe kimapambano
Kama nifavyo baba yao?”

Basi Nabwa, baba yetu
Kaondoka akikhofu
Lau wanawe twaweza
Kupambana kama yeye
Mbele ya vitisho vile
Mbele ya idhilali ile
Mbele ya gharama zile
Jabir, Ghassani, Salma,
Ali, Jussa, Bimani na Hamza
Wanawe, bila ya yeye, tutaweza?

Tutaweza kusimama kulinda kauli yetu?
Tusiogope lawama wala fitina za watu
Za kuvuliwa uraia, na kupokwa paspoti
Za kuzuiwa riziki kwa kufungiwa milango
Za kugeukwa na hata watu wa karibu
Hivi sisi, wanawe, tutaweza?

Kama tukikoseshwa ajira na pesa ya matumizi
Tukawa twarudi majumbani, paka jikoni kalala
Na kosa letu ni kuwa:
Tumefuata nyayo za baba
Kusema la kweli na lilo la haki
Wanawe tutasubiri na kisha twende pamoja__
Tusigeuze shingo zetu na kumeza matapishi?

Khofu za baba si kwamba
Alituona dhaifu
Lakini dunia hii
Aliona ikichenji
Na mambo yakijipinda
Mbele nyuma; nyuma mbele
Na yeye alitamani azidishe kutufunda
Tuhitimu somo hili
La dhati ya mapambano
Illa sasa amekwenda, akilia:
“Wanangu, Mola, wanangu!”

Naam, ndio sisi wanawe
Katika fani ni yeye aliyetutotoa
Alotuzaa, alotulea, alotukuza
Akatuonesha wapi tusimame na wapi tukae
Wapi tuseme, wapi tunyamae
Na juu ya yote:
Alitufunza heshima na utukufu wa mtu
Kwamba ni kujiamini
Na asojiamini hana utu

Nasi twaona fahari
Kuwa Nabwa baba yetu
Kwamba ndiye mlezi wetu
Kunasibishwa na yeye
Kwetu ni jambo akhasi
Na kiapo chetu ni hiki:
Kama baba kama mwana!

Nabwa, baba, hukujijenga wewe
Uliyojenga ni taasisi
Nitaiita Unabwa
Unabwa ulitufungua midomo
Leo hakuna wa kuifunga
Unabwa ulifungua milango
Ya habari, ya kujieleza na kuelezwa
Wale jamaa wameshindwa kuifunga
Mwangwi wa Dira yako
Ungenasi hadi leo
Ulikuwa taasisi
Na taasisi hudumu!

Basi wewe, baba, fika mbele ya Molao
Jasho ukitiririka
Hilo si jasho la wizi
Ni jasho la kutumika
Kutumikia watuo
Kutumikia faniyo
Kutumia ulezio
Nao ni sisi wanao.

Tungetaka ubakie daima dawamu
Illa madhali mwito wa Mola umeita
Ni shuruti uitikwe
Nawe baba umeuitika
Basi nenda kwa salama
Mithali waja wendao
Wanao ulotuwacha nyuma yako
Usitusikitikie
Tutapambana kijanadume
Na tutakufa tungali watu.

Wanao, baba, wanao
Twakupa ahadi hii:
Tutakufa tungali watu
Hatujageuka nguruwe
Hatutakufa nyamamwitu
Azaaye na wanawe
Tutakufa tukumbukwe
Kama ukumbukwavyo wewe
Kwa heshima, kwa staha na kwa jina
Tutakufa na Unabwa!

No comments: